Ripoti mpya ya Kundi la Wataalamu wa Umoja wa Mataifa kuhusu hali ya usalama katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) inasema kuwa wapiganaji wa RED-Tabara na FNL wamehamisha maeneo yao ya operesheni hadi vilima vinavyoitazama Sange, karibu na mpaka wa Burundi. Kwa mujibu wa ripoti hiyo, hatua hiyo, pamoja na ushirikiano wao na Alliance Fleuve Congo/Mouvement du 23 mars (AFC/M23), Twirwaneho na Jeshi la Rwanda (RDF), imeongeza wasiwasi wa mamlaka za Burundi kuhusu usalama wa nchi. (Le Mandat)
Ripoti inaeleza kwamba makundi hayo mawili ya waasi wa Burundi, Résistance pour un État de droit au Burundi (RED-Tabara) na Forces Nationales de Libération (FNL), yalizidi kushirikiana na muungano unaojumuisha AFC/M23, kundi la Twirwaneho na Jeshi la Rwanda (RDF) kadiri mgogoro wa AFC/M23 ulivyoenea katika jimbo la Kivu Kusini.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, tangu mwaka 2023 makundi hayo mawili ya Warundi yamekuwa yakilengwa na operesheni za pamoja za kijeshi zinazofanywa na Jeshi la Burundi (FDNB) pamoja na Jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (FARDC).
Mikakati ya kujipanga upya baada ya kuondoka Uvira
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, AFC/M23 na RDF zilifanya mabadiliko ya kimkakati ya nafasi zao baada ya kujiondoa katika mji wa Uvira.
Wataalamu hao wanasema kuwa licha ya Marekani kutoa wito katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwa AFC/M23 na RDF kujiondoa angalau kilomita 75 kaskazini mwa Uvira, vikosi hivyo vilijiondoa hadi Sange, takribani kilomita 35 kutoka Uvira, ambako AFC/M23 iliweka makao yake makuu ya shughuli zake katika Kivu Kusini.
Kwa mujibu wa wataalamu hao, hatua hiyo haikuwa kujiondoa kikamilifu bali ilikuwa ni kujipanga upya kijeshi kwa lengo la kuendelea kudhibiti maeneo yenye umuhimu wa kimkakati karibu na Uvira pamoja na maeneo ya vilima vya Moyens Plateaux na Hauts Plateaux, ili kuhifadhi uwezo wa kuendelea na operesheni za kijeshi.
Ripoti hiyo pia inaeleza kuwa kikosi kimoja kilitumwa katika Hauts Plateaux ili kuimarisha wapiganaji wa Twirwaneho na RED-Tabara, huku vikosi vingine vikijipanga upya katika maeneo ya Uvira, Sange na Makobola.
Operesheni za kijeshi zilizofanywa kwa pamoja
Kwa mujibu wa wataalamu hao, RED-Tabara na FNL zilishiriki katika operesheni kadhaa za kijeshi pamoja na AFC/M23, Twirwaneho na RDF katika kipindi kinachozungumziwa na ripoti hiyo.
Ripoti inaeleza kuwa muungano huo ulidhibiti maeneo kadhaa muhimu katika mhimili wa Mwenga–Fizi, yakiwemo Point Zéro, Kanguli na Tuwe Tuwe, huku ukiendelea na operesheni ndani na karibu na Minembwe katika miezi ya Januari na Februari 2026.
Ripoti hiyo pia inasema kuwa RED-Tabara ilikuwa na kambi za muda mrefu katika Masango (wilaya ya Uvira), pamoja na Magunda na Kipupu (wilaya ya Mwenga).
Ingawa viongozi wa RED-Tabara wamekuwa wakikanusha mara kwa mara kuwa na uhusiano na AFC/M23, wataalamu hao wanasema kuwa wapiganaji wa RED-Tabara walishiriki katika mapigano pamoja na AFC/M23, Twirwaneho na RDF katika maeneo mbalimbali, yakiwemo Muranvia, Bijabo na kwenye njia zinazoelekea Minembwe.
Ripoti hiyo pia inaeleza kuwa wapiganaji wa FNL walikuwepo katika msitu wa Nyaburunda ulioko wilaya ya Uvira, pamoja na maeneo ya milimani karibu na Sange. Katika eneo la Magunda, walikuwa wakitumia kambi pamoja na vikosi vya RED-Tabara.
RED-Tabara na FNL zasogea karibu na mpaka wa Burundi
Kwa mujibu wa wataalamu hao, kufikia katikati ya Februari 2026 wapiganaji wa RED-Tabara na FNL walikuwa tayari wamejiunga moja kwa moja na muungano wa AFC/M23, RDF na Twirwaneho katika sekta ya Kamombo, iliyoko katika Hauts Plateaux.
Ripoti inaongeza kuwa wapiganaji wengine wa makundi hayo waliondoka katika maeneo ya Fizi, Uvira na Mwenga na kuelekea kwenye vilima vinavyoitazama Sange, karibu kabisa na mpaka wa Burundi.
Kwa mujibu wa wataalamu hao, ukaribu wa makundi hayo ya waasi na mpaka wa Burundi, pamoja na ushiriki wao katika operesheni za kijeshi sambamba na AFC/M23 na RDF, umeongeza wasiwasi wa mamlaka za Burundi, ambazo zinahofia kuwa makundi hayo yanaweza kutumiwa kuiyumbisha Burundi.
Mpaka wafunguliwa tena huku ulinzi ukiimarishwa
Ripoti inaweka hatua zilizochukuliwa na Serikali ya Burundi katika muktadha wa hali ya kijeshi iliyokuwa ikiendelea Uvira na pembezuni.
Baada ya AFC/M23 kuuteka mji huo mwezi Desemba 2025, Burundi ilifunga vituo kadhaa vya mpakani na DRC na kutangaza baadhi ya maeneo ya mpakani kuwa maeneo ya kijeshi, kutokana na kuzorota kwa hali ya usalama.
Wiki chache baadaye, baada ya AFC/M23 kujiondoa Uvira, Burundi ilifungua tena baadhi ya vituo vya mpakani tarehe 25 Februari 2026, ikitaja sababu za kiuchumi, kibinadamu na kiutendaji.
Hata hivyo, wataalamu hao wanasisitiza kuwa hatua hiyo haikumaanisha kuwa wasiwasi wa kiusalama ulikuwa umepungua.
Badala yake, walieleza kuwa ilikuwa ni mpito kutoka hatua za dharura za kufunga mpaka kwenda katika mfumo wa ulinzi ulioimarishwa, ukiwa na doria zaidi, ongezeko la wanajeshi katika maeneo muhimu ya kuvuka mpaka na udhibiti mkali zaidi wa shughuli za kuvuka mpaka.
Madai ya uandikishaji na mafunzo nchini Rwanda
Ripoti hiyo pia inaeleza kuwa RED-Tabara imekuwa na uhusiano wa muda mrefu na Rwanda pamoja na Jeshi la Rwanda (RDF).
Kwa mujibu wa wataalamu hao, uandikishaji wa wapiganaji wa kundi hilo la RED-Tabara uliendelea katika kambi za wakimbizi nchini Rwanda, hasa kambi ya Mahama. Baadaye, wataalamu hao wa Umoja wa Mataifa wanasema kwamba waandikishwa hao walipelekwa katika vituo vya kijeshi vya Gako, Gashora na Gabiro, ambako walipatiwa mafunzo ya kijeshi.
Soma pia hii Burundi: Seif Ntakamurenga afariki dunia baada ya kupigwa vikali na Imbonerakure
